Header Ads

PropellerAds

Breaking News

WAFANYABIASHARA NGUZO ZA UMEME WALIA KUTOLIPWA STAHIKI ZAO


Wasambazaji wa nguzo katika kiwanda cha SAO Hill cha wilayani Mufindi kinachoendeshwa na kampuni ya Green Resources Ltd. wameilalamikia kampuni hiyo kushindwa kuwalipa fedha za mauzo ya nguzo kwa wakati hali inayosababisha wasambazaji hao kushindwa kuendesha biashara zao huku mali zao zikiwa hatarini kufilisiwa na taasisi za mikopo.
Baadhi ya wasambazaji waliokutwa kiwandani hapo wakisubiri kuonana na uongozi wa kampuni ya SAO Hill Industries inayomilikiwa na kampuni ya Green Resources wamesema makubaliano waliyoingia na kampuni hiyo ni kulipwa fedha zao mara wanapofikisha magogo kiwandani hapo jambo ambalo lilitekelezwa mpaka mwezi Septemba mwaka huu.

Aidha wafanyabiashara hao wamelalamikia makato ya asilimia tano kwaajili ya ushuru wa halmashauri wanayokatwa kwenye malipo yao na kampuni ya SAO Hill Industries licha ya wao kuwa wamekwishalipia na kuongeza kuwa wanapojaribu kuonana na uongozi wa kampuni hiyo wamekuwa wakizuiliwa getini hivyo kushindwa kujua hatma ya malipo yao.
Meneja mkuu wa kapuni ya SAO Hill Industries Bw Beatus Bahati amekiri kampuni hiyo kudaiwa na wasambazi hao wa nguzo na kueleza kuwa kampuni imeshindwa kuwalipa kwa wakati kutokana na wateja wake wakubwa wakiwemo shirika la umeme nchini TANESCO kuchelewesha malipo yao huku mauzo ya mbao na nguzo yakiwa yameshuka kwa kiasi kikubwa.