Header Ads

PropellerAds

Breaking News

NI RONALDO MFALME WA SOKA DUNIANI 2016, ABEBA BALLON D'OR YA NNE

MRENO Cristiano Ronaldo amekamilisha mwaka mzuri kwa kushinda tuzo ya Mwanasoka Bora wa Dunia, maarufu kama Ballon d'Or mjini Paris, Ufaransa usiku wa Jumatatu hiyo ikiwa ni mara ya nne kwake.
Mshambuliaji huyo wa Real Madrid amejikusanyia kura 173 za Waandishi wa Habari duniani ili kupeleka nyumbani kwake tuzo hiyo inayotolewa na jarida la soka Ufaransa, ingawa hakuwepo mwenyewe kupokea tuzo yake kwwa sababu yupo kwenye Klabu Bingwa ya Dunia ya FIFA nchini Japan.
Kwa ushindi huo, Ronaldo amewapiku mpinzani wake mkubwa, Lionel Messi wa Barcelona na mshambuliaji wa Atletico Madrid, Antoine Griezmann, waliofuatana nafasi ya pili na ya tatu.

Cristiano Ronaldo ameshinda tuzo ya Mwanasoka Bora wa Dunia kwa mara ya nne

Ronaldo, ambaye sasa anazidiwa tuzo moja tu na Messi anayeshikilia tuzo tano za rekodi za Ballon d'Or, alitabiriwa ushindi huo kutokana na kutwaa mataji Euro 2016, Ligi ya Mabingwa na Super Cup ya UEFA.
Mchezaji huyo wa zamani wa Manchester United sasa anawapiku pia Marco van Basten, Michel Platini na marehemu Johan Cruyff, walioshinda mara tatu kila mmoja tuzo hiyo.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 31 alisema baada ya ushindi huo; "Sikufikiria kushinda tuzo hii mara nne," alisema na kuongeza; "Nimefurahi sana. Nilipotwaa mara ya kwanza nilikuwa nina furaha kupitiliza. Lakini leo najisikia kama nilivyofanya mwaka 2008,".
Ronaldo amefunga mabao 51 katika mechi 55 za klabu na nchi yake mwaka 2016, lakini ni mafanikio katika mashindano mawili makubwa kwa mwaka huu yanamfanya ampokonye tuzo hiyo Messi.
Alitoa mchango mkubwa kwa Real kuwafunga mahasimu wao Atletico Madrid mwezi Mei ili kutwaa taji la Ulaya kwa mara ya 11 na ya rekodi. Miezi miwili baadaye, akaisaidia Ureno kubeba Kombe la Euro 2016 nchini Ufaransa ingawa hakumaliza mchezo wa fainali baada ya kuumia.